Watu 22 kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Burundi na Visiwa vya Comoro wameokolewa katika Wilaya ya Mafia baada ya boti waliyokuwa wakisafiria kuelekea Kisiwa cha Mayotte kupata hitilafu katikati ya bahari, huku watu 14 wakipoteza maisha. Akitoa taarifa leo Julai 24, 2026, Mkuu wa Wilaya ya Mafia, Aziza Mangosongo, alisema tukio hilo lilitokea Julai 22 baada ya boti hiyo, yenye injini aina ya Yamaha na isiyokuwa na usajili, kushindwa kuendelea na safari yake na kupeperushwa hadi kufika katika fukwe za Kijiji cha Kungwi, Kata ya Baleni. Alisema boti hiyo ilikuwa imeondoka Visiwa vya Comoro ikiwa na jumla ya abiria 36 waliokuwa wakielekea Kisiwa cha Mayotte, ambapo walitarajia baadaye kuingia nchini Ufaransa wakisaka usalama kutokana na migogoro katika nchi zao pamoja na kutafuta maisha bora.
Kwa mujibu wa Mangosongo, manusura 22 waliokolewa na kupewa huduma za kwanza kabla ya kuhamishiwa Hospitali ya Wilaya ya Kilindoni kwa ajili ya matibabu. Waliookolewa ni wanaume tisa, wanawake wanane na watoto watano, wakiwemo wavulana watatu na wasichana wawili. Aliongeza kuwa Serikali ya Wilaya ya Mafia kwa kushirikiana na Timu ya Maafa ya Wilaya na wadau mbalimbali imeendelea kuwahudumia manusura hao kwa kuwapatia chakula, mavazi na mahitaji mengine muhimu.
Mkuu huyo wa Wilaya pia aliwapongeza viongozi wa Kijiji cha Kungwi, wananchi na timu za uokoaji kwa kutoa taarifa na kuchukua hatua kwa haraka zilizowezesha kuokoa maisha ya manusura hao. Aidha, aliwataka wananchi kufuata sheria na taratibu za usafiri wanaposafiri kutoka nchi moja kwenda nyingine na kuepuka safari zisizo salama ambazo zinaweza kuhatarisha maisha yao.

